Vyeti vyamuondoa mhudumu wa mochwari


Rais John Magufuli na Makamu wa Rais, Samia
Rais John Magufuli na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan (wa pili kushoto) wakifurahia taarifa ya uhakiki wa vyeti kwa watumishi wa umma, baada ya kukabidhiwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Angellah Kairuki (kulia) mkoani Dodoma hivi karibuni. Wa pili kulia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene.  
Sakata la vyeti fedha limemuondoa kazini mhudumu wa chumba cha kuhifadhia maiti wa hospitali ya Mkoa wa Shinyanga baada ya kukutwa na cheti cha kughushi.
Katibu tawala wa Shinyanga, Albert Msovela amemtaja mtumishi huyo kuwa ni Christopher Lwambo na kusema kuwa ndiye pekee katika hospitali hiyo aliyebainika kuwa na cheti feki.
Msovela amesema hakuna mtumishi mwingine wa umma katika taasisi hiyo aliyenaswa na cheti bandia na kwamba, huduma zinaendelea vizuri.
Wakati mtumishi huyo akiondolewa, Mwenyekiti wa CCM wilayani Chamwino, Charles Ulanga ambaye ni mratibu wa elimu wa Kata ya Buigiri ameandika barua ya kukata rufaa lakini ametakiwa kuipeleka kwa mwajiri wake ambaye ni mkurugenzi mtendaji wa halmashauri.
“Nilishaandika barua, lakini tulielekezwa kuzipeleka kwa waajiri wetu ambao wao ndiyo watazifikisha kwa wahusika. Mimi nimeshafanya hivyo,” amesema Ulanga.
Jina lake lilikuwa miongoni mwa majina yaliyojitokeza katika orodha ya watumishi wanaodaiwa kughushi vyeti.
Hata hivyo, alijitokeza hadharani na kupinga suala hilo akisema alisoma elimu ya msingi na baadaye ualimu bila ya kupitia elimu ya sekondari na kuwa ndivyo vyeti alivyowasilisha.
Wakati Ulanga akikata rufaa, Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (Talgwu) mkoani Morogoro kimepokea wafanyakazi zaidi ya kumi wakilalamikia kutotendewa haki.
Katibu wa Talgwu mkoani humo, Lawrence Mdega amesema wafanyakazi hao walifika ofisini kwake wakilalamika kuwa waliajiriwa kwa elimu ya darasa la saba, lakini wanashangaa wameandikwa kuwa walimaliza kidato cha nne.
Mkuu wa kitengo cha utawala na fedha wa Chuo Kikuu cha Sokoine (Sua), Yonica Ndaga amesema watumishi watatu wa chuo hicho wameonyesha nia ya kukata rufaa wakidai kuonewa na uhakiki uliofanyika ambao haukuwatendea haki.
Share on Google Plus

ABOUT BLOGGER INJILI HALISI MINISTRY

Hi! I am Zachary John Bequeker, from Mwanza Tanzania, East Africa.I'm a blogger of ZAKACHEKA NEWS LINE And ZAKKACHEKA INJILI.Contact me +255 625966236 / +255 758590489 or mail on zacharybequeker@gmail.com . Thanks!!!

0 Post a Comment: